Sunday, April 28, 2013

Bodi ya mikopo yatangaza kuanza kupokea maombi


Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, Bw. Cosmas Mwaisobwa akisisitiza jambo mbele ya waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam alipokua akitangaza kuhusu kuanza kupokea maombi ya mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kuanzia 1 Mei, 2013.

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu imetangaza kuanza kupokea maombi ya mikopo kwa wafunzi wanaotarajiwa kujiunga na Vyuo Vikuu pamoja na wanafunzi wanaoendelea kwa mwaka wa masomo 2013/2014 kuanzia Mei 1, 2013.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Bodi hiyo Bw. Cosmas Mwaisobwa amewaambia waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam kuwa maombi ya mikopo yatafanyika kwa njia ya mtandao kupitia anuani ya http://olas.heslb.go.tz.

Amesema vipeperushi maalum vyenye maelezo ya jinsi ya kuomba mkopo kwa njia ya mtandao vinapatikana kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu, ofisi za Elimu za Wilaya,watoa huduma ya Intaneti, Makao Makuu ya Bodi ya Mikopo na Ofisi za Bodi ya Mikopo za Kanda.

Pia alisema maelezo haya ya mikopo yanapatikana kwenye tovuti ya bodi ambayo ni:www.heslb.go.tz.

Waombaji wapya wanatakiwa kulipa ada ya maombi ya mikopo ya shilingi 30,000/- huku wanafunzi walio katika mwaka wa masomo wa tano au wa sita wa masomo wataendelea kulipa ada ya maombi ya shilingi 10,000/-.

"Wanafunzi wa mwaka wa pili, tatu na nne ambao walilipa ada ya maombi ya shilingi 30,000/- katika miaka ya masomo ya 2009/2010, 2010/2011 na 2011/2012 hawatakiwi kulipa tena ada hiyo ya maombi ya mikopo," alisema.

Bwana Mwaisobwa amesema mwombaji wa mkopo huo anapaswa kuwa na sifa ambazo zimetajwa katika kifungu cha 17 cha Sheria Na 9 ya mwaka 2004 ambazo ni pamoja na na mwombaji kuwa raia wa Tanzania.

Ametaja sifa nyingine kuwa ni kudahiliwa katika chuo cha elimu ya juu, kutokuwa na njia nyingine ya kugharamia elimu ya juu, kufaulu mitihani ya mwaka uliotangulia kwa waombaji wanaoendelea na masomo pamoja na kuwa mhitaji.

"Bodi inasisitiza kwamba waombaji wa mikopo wazingatie muda uliopangwa na pia kufuata kwa umakini taratibu zote zilizoainishwa katika uombaji wa mikopo," alisema na kusisitiza kuwa hakutakuwa na muda wa ziada baada ya muda uliopangwa kupita.

Mwisho wa kupokea maombi hayo ya mikopo ni 30 Juni 2013.

Bodi ya Mikopo ya Elimu ya juu kwa mwaka wa masomo wa 2012/2013 iliwapatia mikopo wanafunzi wapatao 94,703.

No comments:

Post a Comment