Sunday, April 28, 2013

MBUNGE LEMA AZUILIWA KUPIGA MSWAKI WALA KUNYWA CHAI AKIWA MAHABUSU...... !!

TUKIO la kukamatwa na kuwekwa mahabusu kwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema (CHADEMA), kwa madai ya uchochezi, limeibua sura mpya baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutajwa kuwa nyuma ya mkakati huo,

Lema ambaye bado anaendelea kusota rumande siku ya tatu baada ya kunyimwa dhamana, ameanza kufanyiwa vituko na Jeshi la Polisi baada ya jana asubuhi mkewe kuzuiliwa asimpe mswaki wala chai.

Mbunge huyo alikamatwa kutokana na amri ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, aliyedai kuwa aliwachochea wanafunzi wa Chuo cha Uhasibu Arusha kumzomea kiongozi huyo na kupopoa gari lake kwa mawe.

Hata hivyo, siku moja kabla ya kukamatwa Lema aliwaonesha waandishi wa habari ujumbe mfupi wa simu ya kiganjani aliyotumiwa na Mulongo akimtishia kuwa atamfungulia kesi yoyote anayoitaka.

“Umeruka kihunzi cha kwanza, nitakuonesha kuwa mimi ni serikali, ulikojificha nitakupata na nitakupa kesi ninayotaka mimi,’’ ulisomeka ujumbe huo uliotumwa kupitia simu namba 0752 960276 ambayo Lema alidai ni ya Mulungo.

Pia nguvu kubwa iliyotumika kumkamata mbunge huyo usiku saa 5:30 kwa kutumia askari na maofisa wa usalama kuzingira nyumba yake, imehojiwa na baadhi ya wananchi, wakitilia shaka kuwa kuna siri ndani yake.

Madai ya Mulongo kuwa Lema alichochea wanafunzi hao yanakinzana na ushahidi wa video unaoonesha kuwa mbunge huyo alitumia kila aina ya ushawishi kuwasihi wasiandamane baada ya mwenzao, Elly Kago (22), kuuawa na watu wasiojulikana jirani na chuo hicho.

Akizungumza na gazeti hili jana, mke wa Lema, Neema, alisema kuwa alifika kituo cha polisi asubuhi akipeleka chai, lakini akaelezwa kuwa haruhusiwi kumpelekea chai.

Alisema kuwa alipiga simu kwa mkuu wa upelelezi wa mkoa ndipo akaambiwa ampelekee na alipofika tena kituoni askari aliyekuwa zamu alianza kupekua mfuko wa Neema kwa fimbo, kisha akaamuru Lema apewe, ila anywe kwa dakika tatu.

Wakati anafungua chupa ya chai na kumimina kwenye kikombe, askari alimweleza kuwa imebaki dakika moja, hatua iliyomuudhi Lema akidai ni udhalilishaji, hivyo akashindwa kunywa.

Alipotaka kupewa mswakiaskari alikataa kuwa vifaa hivyo vinaweza kutumika kama silaha, hivyo haruhusiwi kupewa.

Tanzania Daima Jumapili lilizungumza na wanasheria kadhaa pamoja na wanasiasa wabobezi kuhusu sakata hilo, ambapo baadhi walidai huo ni mkakati wa CCM kutaka kuidhoofisha CHADEMA katika uchaguzi mdogo wa madiwani ujao kwenye kata nne.

“Kesho mnaweza kusikia Lema akifunguliwa kesi ya ajabu ya kutunga halafu kwa kipindi hiki kampeni zikianza mahakama itakuwa ikiisikiliza mfululizo ili asipate nafasi ya kushiriki kikamilifu.

“Huu mkakati si wa Mulongo peke yake bali ni mbinu za CCM zilizobakia katika kuhakikisha wanaikamata Arusha. Lakini naona kama wanazidi kujimaliza,” alisema mwanasiasa mmoja aliyeomba kuhifadhiwa jina lake.

Mwanasiasa huyo kutoka mkoani Arusha aligusia pia mkanganyiko wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) hivi karibuni kutangaza kata nne kurudia uchaguzi na kuiacha moja ya Sombetini ambayo diwani wa CCM alihamia CHADEMA.

“Ujue CCM wanafanya mambo bila kupima athari, Arusha ni mji wa kitalii lakini kwa sasa unaogopeka kwa fujo za polisi na wanasiasa, hata kesho utaona wakati Lema akipelekwa mahakamani.

“Hapa ni ngome ya CHADEMA hata kama Lema hayupo, sasa NEC wameibana Sombetini kwa hofu kuwa kata zote zikienda CHADEMA watakuwa na madiwani zaidi ya CCM, hivyo ishu ya meya kufufuka upya, ndiyo wakaamua kumtumia Mulongo kufanya mchezo huu wa hatari,” alisema.

Alipopigiwa simu jana jioni na kuulizwa juu ya madai hayo, Mulongo alizungumza kwa ukali akisema:“Wewe mhariri unaweza kunipigia simu kuniuliza swali kama hilo?”..

Aliendelea kufoka akisema: “Acheni kufanya kila kitu siasa, wewe ni polisi kujua Lema kwanini akamatwe hivyo, niache mimi niko na wageni wangu,” alisema na kukata simu.

Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Francis Stolla, alizungumzia suala la kukamatwa kwa Lema akisema kuwa nguvu kubwa na utaratibu uliotumika kumkamata haukuwa wa busara.

Stolla alisema: “Kwa mujibu wa kifungu cha 58 na 59 vya sheria ya ushahidi, Jeshi la Polisi au hata kama ni kwa amri ya mkuu wa mkoa ya kukamata walipaswa kuchagua njia nyingine ya busara.

“Jeshi linaweza kuwa na mamlaka mapana ya kukamata au hata kama ni kwa amri ya mahakama, busara huhitajika kutumika. Lema ni mbunge, anafahamika na upatikanaji wake hauna utata, anapotuhumiwa kuhitajika polisi busara inatumika kumwita au kumwandikia aende, si kumvizia kama walivyofanya,” alisema.

Mwanasheria mwingine ambaye aliomba kuhifadhiwa jina, alifafanua kuwa: “Rais peke yake ndiye Amiri Jeshi. Uamiri jeshi wa rais haugawanyiki mpaka kwa wakuu wa mikoa.

“Uamiri jeshi wa rais upo kikatiba, hauwezi kuwa wa wakuu wa mikoa au wa wilaya. Ndiyo maana anayeamrisha polisi katika mkoa ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa, na wilayani anakuwapo ofisa anayeamrisha (OCD),” alisema.

Aliongeza kuwa sheria zinaruhusu mkuu wa mkoa na wilaya kutoa amri ya kukamata mtu kama hakuna askari lakini mtuhumiwa anapokamatwa sharti aambiwe anakamatwa kwa kosa lipi na anayemkamata ajitambulishe.

Alisema kuwa siku ya tukio chuoni, polisi walikuwapo wakati Lema akizungumza na wanafunzi na hawakuona kosa lolote kwake ndiyo maana hawakumkamata, sasa iweje mkuu wa mkoa aje na amri.

Akizungumzia nguvu iliyotumika katika kumkamata Lema, Mwenyekiti wa Baraza la Vijana CHADEMA (BAVICHA) Mkoa wa Tanga, Aaron Mashuve, aliliomba Jeshi la Polisi kuelekeza nguvu kama hizo katika kusaidia watu wenye ulemavu wa ngozi (albino).

Alisema nguvu hiyo kama ingetumika wauaji hao wangekuwa wamekamatwa badala ya polisi kupoteza muda kuhangaika na wanasiasa ambao wanaweza hata kuitwa kituoni wakaenda kwa hiari yao.

Katika hatua nyingine, CHADEMA mkoani Arusha kimetangaza kumfungulia mashtaka mkuu wa mkoa huo kwa tuhuma za kumtishia mbunge wao kwa ujumbe wa maandishi, pia kumtaka athibitishe madai ya kuwa kifo cha mwanafunzi kina uhusiano na masuala ya kisiasa.

Katibu wa mkoa wa chama hicho, Amani Golugwa, alisema taratibu za kuyashughulikia masuala hayo yote mawili zinaendelea chini ya jopo la wanasheria wa chama hicho.

No comments:

Post a Comment