Saturday, May 18, 2013

Machozi ya wanamuziki na hatima ya muziki wa Tanzania

Hivi karibuni wanamuziki wa kizazi kipya, wameibua malalamiko kwa waliokuwa mapromota katika shughuli za muziki.

Kimsingi kinacholalamikiwa ni kunyonya au kuingiliwa katika kazi zao za muziki.

Nisingependa kujiingiza kwa undani kwenye malalamiko hayo, lakini kama mpenzi wa muziki wa Tanzania nimeona kuna haja ya kuangalia hatima ya muziki huu ikiwa ni pamoja na maendeleo ya wanamuziki wenyewe.

Kwanza niseme kwamba malalamiko yanayowakilisha kilio cha wanamuziki wengi nchini yanaweza kuwa chanzo cha muziki wetu kudumaa.

Tukubali kwamba fani ya muziki nchini iko katika hali mbaya, hasa kwa kuwa wanamuziki wengi ni maskini kwani hawafaidiki na sanaa yao. Tatizo lililopo ni mfumo mbovu wa kuwawezesha wasanii hao kujitegemea kiuchumi.

Tukiangalia maendeleo ya muziki tangu wakati wa kupata uhuru mwaka 1961, tunaona mabadiliko mengi ya kisiasa yaliyofanywa na Mwalimu Julius Nyerere katika uongozi wake, yaliathiri pia fani ya muziki nchini.

Mkakati wa Mwalimu Nyerere kuunda Serikali dola inayomiliki kila kitu, kuliwanyima uhuru wasanii wengi wa muziki.

Kwa hali hiyo bendi nyingi zikabaki kumilikiw na mashirika ya umma. Mfano ni Bima Lee Orchestra iliyokuwa chini ya Shirika la Bima, DDC Mlimani Park iliyokuwa chini ya Shirika la Maendeleo la Dar es Salaam, Nuta, Juwata na baadaye OTTU ilikuwa ikimilikiwa na Jumuiya ya Wafanyakazi nchini, na nyinginezo nyingi.

Kutokana na hali hiyo, wanamuziki walikuwa wakitegemea kulipwa mishahara kila mwezi kama wafanyakazi wengine wa mashirika hayo. Hawakuwa na mikakati binafsi ya kujiongezea kipato nje ya mashirika hayo. Haishangazi kuona kuwa muziki wa dansi uliokuwa ukitamba miaka ya 1970/80 na 90 mwanzoni ulidumaa na kushindwa kuvuka mipaka ya nchi.

Baadhi ya wanamuziki hawakuridhika na hali hiyo, wakakimbilia Nairobi Kenya kutafuta maisha. Wapo kina John Ngereza, Issa Juma, Joseph Just, Mohammed Tika Abdallah Victor Boniface walioungana na wanamuziki wa Kenya kuunda Kundi la Les Wanyika.

Wengine ni pamoja na Mbaraka Mwinshehe na bendi yake ya Super Volcano, aliyependelea kurekodi nyimbo zake Nairobi. Wengine walikwenda huko, lakini hawakuvuna na walirudi tena nchini.

Baada ya kuanguka kwa mfumo wa Ujamaa na Kujitegemea ulioasisiwa na Mwalimu Nyerere, bendi hizo nyingi zikaanza kujitegemea. Lakini hazikufika mbali kwani wanamuziki wengi walikuwa wamezeeka huku muziki wa kizazi kipya (Bongo fleva) ukiibuka kwa kasi.

No comments:

Post a Comment