Saturday, May 18, 2013

SIKU CHACHE BAADA YA MLIPUKO ARUSHA, WATU WATANO WAKAMATWA DAR NA MILIPUKO. STORI NZIMA HII HAPA

POLISI katika Kanda Maalumu ya Dar es Salaam inawashikila watu watano kwa tuhuma za kupatikana wakiwa na milipuko hatari.
Akizungumza leo, Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo, Suleiman Kova alisema watuhumiwa hao walikamatwa katika msako mkali unaoendelea kufanywa na askari polisi katika maeneo ya Kunduchi jijini humo.
Aliwataja waliokamatwa kuwa ni Juma Khalfani (24), Reuben Patrick (26), Happy Charles (28), Sadick Seif (32) na Iddi Shaaban (40), wote wakazi wa Kunduchi Mtongani katika Manispaa ya Kinondoni.
Alisema kukamatwa kwa watuhumiwa hao kunatokana na taarifa walizozipata kutoka kwa raia wema. Kova alisema watuhumiwa hao walikamatwa wakiwa na nyaya 62 za milipuko zikiwa zimefungwa betri, vifaa nane vya kusababisha milipuko, nyaya ndefu mizunguko minne, 'tube' 20 za urefu wa sentimita 30 zilizojazwa mbolea ya urea na tambi rola moja.
Alisema katika operesheni hiyo pia wamefanikiwa kukamata gari lenye namba za usajili T 772 BYC aina ya Noah pamoja na pikipiki ya miguu mitatu yenye namba T 959 BTE zikiwa kwa mtuhumiwa Sadick Seif ambae alishindwa kuthibitisha uhalali wa umiliki wake.
Aidha alisema kuwa uchunguzi wa tukio hilo utakapokamilika jalada lake litapelekwa kwa mwanasheria mkuu wa serikali kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria.

No comments:

Post a Comment