Tuesday, May 21, 2013

Dr. Slaa amuonya vikali Spika Anne Makinda




 
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa, amesema ikibidi Bunge livunjike au wabunge wa chama hicho wafukuzwe bungeni, lakini hawako tayari kuzibwa mdomo kuzungumzia masuala yanayohusu maisha ya Watanzania. Amesema chama hicho hakitakubali wabunge wake wapangiwe mambo ya kuzungumza kwa kutegemea busara za Spika au Naibu Spika, bali wataangalia na kufuata maelekezo ya kanuni za Bunge, akisema ndiyo msingi wa uendeshaji wa chombo hicho cha uwakilishi wa wananchi.

Akizungumza katika mikutano ya hadhara iliyohudhuriwa na maelfu ya watu jana katika maeneo ya Ngalangala, Basotu, wilayani Hanang na Haydom, wilayani Mbulu, kuhusiana na hotuba ya Sugu kuahirisha Bunge, Dk. Slaa alisema wabunge wa chama hicho daima wataendelea kuwasemea Watanzania wanyonge ndani na nje ya Bunge. “Moja ni tukio lililotokea leo (jana) bungeni. Kwa wale mliofuatilia mkutano wa Bunge mliona kilichotokea. Ninachotaka kumwambia Spika na wasaidizi wake bungeni ni kwamba Bunge linaongozwa kwa kanuni za bunge, si vinginevyo.

Uamuzi aliofanya wa kuagiza hotuba ya wabunge wetu ipelekwe kwenye Kamati ya Maadili ya Bunge ni kinyume na kanuni ambazo ndizo msingi wa utendaji kazi wa bunge. Hakuna sehemu yoyote katika kanuni inampatia mamlaka Spika ya kupeleka hotuba ile kwenye kamati hiyo, ili waelekeze nini kisemwe. Hakuna,” alisema Dk. Slaa huku akishangiliwa na umati mkubwa wa watu.

Alisema kuwa baada ya mawasiliano ya viongozi wa juu wa chama hicho na uongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, walikubaliana kuwa kwa sababu hotuba hiyo haikuvunja kanuni yoyote ile ya Bunge, hawatakubali kuondoa au kupunguza neno hata moja.

Source:Nipashe Jumanne.

No comments:

Post a Comment